Social Icons

Monday, October 17, 2016

RC: Wanafunzi Mbeya Day wanavuta bangi


MKUU wa Mkoa wa Mbeya, Amos Makalla amesema, wanafunzi wengi wa shule ya Kutwa Mbeya, wanavuta bangi katika eneo la shule ya msingi Azimio na huwafanyia fujo walimu.
Akizungumza katika kituo cha redio, Makalla alisema uongozi wa mkoa umeiagiza bodi ya shule, ichukue hatua ya kurejesha nidhamu katika shule hiyo kwa kuwa haiwezekani mwanafunzi kuwa juu ya mwalimu.
Alisema adhabu iliyotolewa ni kubwa, lakini lipo tatizo la wazazi kushabikia mambo kwa kutetea watoto wanapokosea, aliwataka wazazi wasiwashabikie watoto kwa kuwa wanatengeneza kizazi kisichokuwa na malezi mazuri.
"We jiulize kwamba je wanafunzi wale walioko pale wananidhamu ya kutosha na walimu ndio chanzo? Wakati tukio hili linaendelea kuchunguzwa na Polisi, hali ya nidhamu kwa wanafunzi wa kidato cha tatu na cha nne wa Mbeya Day (Shule ya Kutwa Mbeya) ni mbaya.
Kwa hiyo serikali lazima ichukue hatua ya kurejesha nidhamu kupitia bodi ya shule lazima tushirikiane kurejesha nidhamu, kuna watoto pale, tayari tunayo majina ya watoto wanakwenda kuvuta bangi shule msingi Azimio, wakifika pale ni kufanya vurugu, kwa hiyo tunachukua hatua ya kurejesha hiyo nidhamu," alisema Makalla.
Alisema wakati mambo mengine ya miongozo na taratibu za Wizara ya Elimu yakiendelea, uchunguzi wa vyombo vya dola utaendelea. Alisema hataki jambo kama hilo litokee tena na kutaka ifike mahali wanafunzi wengine wasiweze kuwafanyia fujo walimu.
Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi Profesa Joyce Ndalichako amesema ni muhimu kusimamiwa na walimu na mwanafunzi mwenyewe kujenga mazingira kwamba haendi shule kwa ajili ya kuadhibiwa bali kusoma.
Alisema malezi yanaanzia kwa wazazi, hivyo ikiwa wazazi nao hawatekelezi wajibu hao, huchangia kwa kiasi kikubwa kuporomoka kwa maadili na nidhamu kwa watoto.
Alisema pamoja na kwamba adhabu ile haikustahili, lakini lipo tatizo kubwa kwa wanafunzi kutokuwa na nidhamu kwa walimu, jamii na wenzao.
Alisema mwalimu anapaswa kutambua kuwa ameingia kwenye kundi la walezi, hivyo kujenga ukaribu na mwanafunzi na kumsaidia kwa kusimamia ipasavyo nidhamu na si kuweka mbele adhabu. Neno la Ten/Met Shirika la Ten/Met pamoja na kulaani ukatili aliofanyiwa mwanafunzi huo, pia lilishauri mifumo ya elimu ya ualimu na malezi ya wanafunzi iimarishwe.
Mratibu wa Ten/Met, Cathleen Sekwao alisema huenda haiba ya uchaguzi wa aina ya wanafunzi wa kusoma ualimu, haizingatiwi vya kutosha siku hizi.
"Matokeo ni kwamba watu wasio na haiba ya ualimu hujiunga na kozi ya ualimu na kufanya yasiyostahili. Huenda pia mtaala wa mafunzo ya ualimu unakazia zaidi masomo kuliko malezi," alisema Sekwao katika tamko lake juzi.
Alipendekeza wanafunzi wanaochaguliwa kuingia ualimu, wapendekezwe na shule wanakomalizia elimu ya sekondari na mtaala wa elimu ya ualimu, uangaliwe upya hasa kipengele cha malezi ya wanafunzi, maadili na muongozi wa uhusiano baina ya mwalimu na mwanafunzi.
Aidha, alipendekeza Chama cha Walimu Tanzania (CWT) kutoa mafunzo ya mara kwa mara kujenga uhusiano kati ya mwalimu na mwanafunzi.
Awali, akizungumza na gazeti hili, Rais wa CWT, Gratian Mukoba alisema walimu vijana wa sasa wamekosa kujitambua kuwa wanapokuwa walimu wanaingia katika kundi la walezi, hivyo wanapaswa kulea zaidi ya kufikiria kuadhibu.
Mukoba alisema adhabu ni hatua ya mwisho kwa mwanafunzi na kushauri walimu kujenga ukaribu na wanafunzi katika misingi ya kutaka kujua tatizo linalomfanya mwanafunzi kuwa na tabia mbaya na sugu.
Aliwataka walimu vijana kuweka kando mihemuko, kutumia miongozo na sheria katika kufanyakazi zao kwa weledi, badala ya kugeuka mabondia na vituko kwa jamii hivyo kusababisha wanafunzi kutowaheshimu.
Utoaji wa viboko Wakati hayo yakibainishwa, Serikali imesema Waraka wa Elimu wa mwaka 2002 unaelekeza utoaji wa adhabu ya viboko kwa wanafunzi kuwa ni lazima kuidhinishwa na mwalimu mkuu kwa maandishi, huku kukiwa na daftari linaloonesha idadi ya viboko, alivyopigwa mwanafunzi na mwalimu aliyemchapa.
Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi imeweka bayana utoaji wa adhabu hiyo, lakini wakiwataka wanafunzi kujiepusha kufanya makosa mbalimbali, yatakayosababisha kupigwa viboko kwani shuleni wameenda kwa ajili ya kusoma.
Kaimu Kamishna wa Elimu, Nicholaus Buretta alisema hayo juzi alipozungumzia Waraka huo Namba 24 wa mwaka 2002, ulioanza kutumika Desemba Mosi mwaka jana, unaoelekeza adhabu zinazopaswa kutolewa kwa mwanafunzi kwa utovu wa nidhamu uliokithiri au kufanya makosa ya jinai.
Alisema adhabu hiyo ya viboko, hutolewa kwa kuangalia ukubwa wa kosa, jinsi ya mwanafunzi, afya yake pamoja na kuhakikisha viboko hivyo havizidi vinne kwa mwanafunzi, tena hutolewa na mwalimu mkuu au mwalimu aliyethibitishwa na Mwalimu Mkuu kwa maandishi. “Hatuhamasishi adhabu hii kwa wanafunzi bali wanafunzi wanatakiwa kujua kuwa wamekuja shuleni kusoma na hawajaja kuchapwa viboko hivyo lazima wajiepushe kufanya makosa yatakayosababisha kuchapwa.
Tunahamasisha mahusiano bora kati ya mwalimu na mwanafunzi ambayo ni yale ya kama mzazi,” alisema Buretta. Alisema katika mahusiano hayo mtoto anatakiwa kuwa rafiki wa mwalimu bila kukiuka taratibu za ulezi kwa lengo la mwanafunzi asimuone mwalimu wake kama simba ambaye wakati wote anamuogopa. Buretta alisema serikali hivi sasa ina mikakati ya uboreshaji elimu inayowekwa na Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu.
Alisema watahakikisha wanafikia wastani wa darasa moja kuwa na wanafunzi 1:40 hadi 45 ili kufikia malengo. Adhabu ya viboko mashuleni, inasimamiwa na sheria ya adhabu kwa wanafunzi mashuleni ya mwaka 1979. Sheria hiyo ilikuwa inatoa fursa ya mwanafunzi kuadhibiwa viboko visivyozidi sita. Hata hivyo, mwaka 2000 Serikali ilihaulisha sheria hiyo na kuweka idadi ya viboko kwa mwanafunzi visizidi vinne na adhabu hiyo itolewe na mwalimu mkuu.
Imeandikwa na Theopista Nsanzugwanko, Gloria Tesha na Shadrack Sagati
CHANZO GAZETI LA HABARI LEO

No comments:

Post a Comment