Social Icons

Tuesday, August 1, 2017

MAJALIWA: MAJI SAFI SASA KUPATIKANA NCHI NZIMA




Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa
WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amesema serikali (pichani) imedhamiria kumaliza tatizo la upatikanaji wa maji safi na salama katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo Wilaya ya Rungwe mkoani Mbeya ilitengewa Sh bilioni 2.72 kwa ajili ya ujenzi wa miradi ya maji.

Alisema mkakati huo unatekelezwa kupitia Kampeni ya Rais John Magufuli ya kumtua mama ndoo, wananchi katika maeneo yote nchini watapata huduma ya maji safi na salama katika umbali usiozidi mita 400 kutoka kwenye makazi yao. Waziri Mkuu aliyasema hayo juzi alipozungumza kwa nyakati tofauti na wananchi wa halmashauri za Rungwe na Busokelo katika mikutano ya hadhara aliyoifanya Kandete na Tandale katika Wilaya ya Rungwe mkoani Mbeya.
Majaliwa alisema Mkoa wa Mbeya umetengewa Sh bilioni 10.383 kwa ajili ya utekelezaji miradi mbalimbali ya maji, ambazo kati yake Sh bilioni 2.72 zinatarajiwa kutumika katika utekelezaji wa miradi ya maji kwenye Wilaya ya Rungwe. Waziri Mkuu alitaja mradi mwingine unaotekelezwa wilayani Rungwe ni pamoja na mradi wa maji wa Masoko wenye thamani ya Sh bilioni 5.3, utakaohudumia jumla ya vijiji 15.
“Mradi huu ni miongoni mwa miradi inayojengwa chini ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji kwa fedha za ndani,” alieleza. Alisema mradi huo utakapokamilika utawanufaisha wananchi wapatao 19,624 katika vijiji vya Bulongwe, Ngaseke, Igembe, Ntandabala, Lupando, Bujesi, Lufumbi, Nsyasa, Ikama, Itagata, Busisya, Mbaka, Isabula, Lwifa na Nsanga.
Pia Waziri Mkuu alisema wananchi lazima wazingatie Sheria ya Mazingira inayozuia kufanya shughuli za kibinadamu pamoja na kujenga kwenye maeneo yote ya vyanzo vya maji ndani ya mita 60 ili kuliepusha Taifa kugeuka jangwa. Kutokana na hali hiyo, Waziri Mkuu aliwaagiza watendaji kuwachukua hatua watu wote watakaokutwa wakiendesha shughuli mbalimbali kama za kilimo, ujenzi wa makazi na uchungaji wa mifugo ndani ya vyanzo vya maji kwa kuwa zinasababisha ukame.
CHANZO HABARI LEO

No comments:

Post a Comment