Na Mwandishi Wetu
Katika kampeni za takribani siku 60, Rais Magufuli aliahidi mambo mengi yakiwamo ya kusaidia na kuwainua watu wa kipato cha chini na hasa masikini ili kuhakikisha wanapata maendeleo.
Kauli hiyo amekuwa akiitoa kila mara alipokuwa
akirudisha nidhamu serikalini, akitumbua majipu, akiwaajibisha watendaji wabovu na wala rushwa.
Katika
kampeni yake ya kuwainua watu masikini, Rais Magufuli alitoa ahadi ya
kuwainua wananchi hao wanaoishi vijijini kwa kuwapelekea mamilioni,
yanayojulikana kama Mamilioni ya JPM.
Tunapotathmini
mwaka moja wa kuwaongoza Watanzania na kukaa Ikulu ya Magogoni, Ilala,
Dar es Salaam, Rais Magufuli, tunabaini kwamba amekuwa kipenzi na rafiki
wa watu masikini na amekuwa mstari wa mbele kuwatetea wajasiriamali
wadogo.
Ukweli
huo umejidhihirisha kila mahali alipotembelea na kukutana nao, amekuwa
mstari wa mbele kuhakikisha hawabughudhiwi na manispaa, wilaya na
majijini kwa kutozwa kodi zisizoeleweka, kuhamishwa bila kuwaandalia
miundombinu na mazingira rafiki ya kufanyia biashara.
Mfano
mzuri Rais Magufuli ameutoa Julai 18, mwaka huu, wakati akiwaapisha
polisi Ikulu Dar es Salaam, ambapo aliomba wamachinga wasisumbuliwe
katikati ya jiji kwa lengo la kuwataka watafute riziki halali kwa
kutumia biashara zao ndogo.
Rais
Magufuli pia akiwa ziarani mkoani Mwanza, Agosti 12, 2016, aliwaagiza
viongozi wa halmashauri na jiji hilo na Watanzania wote, kutowahamisha
wamachinga, hadi pale halmashauri hizo zitakapokuwa zimeandaa
miundombinu na mazingira rafiki ya kufanyia biashara na shughuli zao za
uzalishaji.
"Hakuna
kuondoa machinga mjini kwani huko nje mnakowapeleka hakuna wateja,”
ilikuwa kauli ya Rais Magufuli iliyopokewa kwa shangwe na umati wa
wakazi wa Mwanza uliofanyika katika Viwanja vya Furahisha.
Kauli
hiyo ya Rais Magufuli, inaeleza wazi kuwa, amekuwa rafiki wa masikini,
wafanyabiashara wadogo, mamalishe, babalishe na wajasiriamali wadogo,
kwani amewataka wafanye shughuli zao za kupatia riziki bila
kubughudhiwa, kusumbuliwa na kuhangaishwa na viongozi wa maeneo husika.
Rais
Magufuli katika kuimarisha urafiki huo na wajasiriamali wadogo ambao
wanatafuta riziki yao kwa kutoa jasho, bila mitaji na kuambulia kipato
kidogo, ameamua kutegua kitendawili cha umasikini wao kwa kutoa Sh
milioni 50 za maendeleo kwa kila kijiji nchini.
Kitendawili
hicho hakika kitateguliwa na Rais Magufuli, kama ilivyo kawaida yake,
ya kutekeleza ahadi nyingi na kwa muda mfupi, hivyo wajasiriamali kwa
ujumla wao, wanatakiwa kuchangamkia fursa hiyo ambayo itatolewa vijijini
kupitia vikundi mbalimbali vya ushirika.
Katibu
Mtendaji wa Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC), Beng'i Issa,
amesema serikali itaanza kutoa fedha hizo kuanzia mwaka ujao wa fedha.
Katika kuhakikisha ahadi hiyo inatekelezwa, Serikali tayari imetenga Sh
bilioni 811, ambazo kabla ya kugawanya vijijini, imejikita katika
kutafuta maoni ya wadau ili kuendesha mchakato huo tija na ufanisi.
Lengo
ni kutorudia makosa yaliyofanyika katika ugawaji wa mabilioni, ambayo
yaliishia katika mifuko ya wajanja. Ili fedha hizo ziwafikie walengwa
katika miradi ya maendeleo yao, maoni ya wadau mbalimbali wa maendeleo
yanatakiwa na wajasiriamali hao kwa kupewa mafunzo ya namna ya
kuanzisha, kuendesha na kudumisha miradi hiyo ya maendeleo.
Walengwa
kabla ya kupata fedha hizo, watapatiwa mafunzo ya ujasiriamali ya namna
ya kutumia fedha hizo ambazo ni muhimu katika kuanzisha, kuendeleza na
kudumisha miradi ya maendeleo.
Serikali
imewakutanisha viongozi wa halmashauri za wilaya, Benki Kuu ya Tanzania
(BoT), Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (Tasaf), benki, mifuko ya hifadhi ya
jamii na vikundi mbalimbali kutafuta namna ya kugawa fedha hizo. "Fedha
hizo zitatolewa kwa awamu tatu katika kipindi cha miaka mitano,”
alisema na kuongeza.
"Fedha
hizo zitatolewa na kupelekwa benki kabla ya kutolewa kwa vikundi
mbalimbali kama Vicoba na Saccos kulingana na taratibu zitakazowekwa."
Mchakato
huo unaanza katika mikoa 10 nchini iliyo nyuma katika kutumia huduma za
kifedha. Mikoa hiyo ni Singida, Lindi, Mtwara, Mbeya, Shinyanga, Geita,
Kagera, Dodoma, Rukwa na Ruvuma. Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu,
Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu, Jenista Mhagama,
amesema kabla ya fedha hizo kugawanywa katika vijiji, lazima kupata
maoni ya wataalamu namna bora ya kutekeleza mpango huo.
Kaimu
Mkurugenzi, Maendeleo ya Sekta Binafsi, Uwekezaji na Uwezeshaji, Ofisi
ya Waziri Mkuu, Victor Mwainyekule, akizungumza kwa niaba ya Waziri
Mhagama, amesema fedha hizo zinatolewa kwa lengo la kupambana na
umasikini.
Mkuu
wa Uendeshaji wa Benki ya Wanawake (TWB), Zablon Yebete, amesema mpango
huo ni uwekezaji mkubwa kwa Watanzania unapaswa kuungwa mkono na vyombo
vya fedha na wadau wengine nchini.
Kabla
ya kutolewa fedha hizo, wamejitokeza matapeli, jambo ambalo Waziri
Mkuu, Kassim Majaliwa amekemea na kuwaonya wananchi kuwa makini na hao
matapeli. Waziri Mkuu, Majaliwa, amewatahadharisha wananchi kuwa makini
na kujiepusha na matapeli wanaopita katika maeneo yao na kuwataka
wachange fedha za kuanzisha vikundi ili wapewe fedha hizo na serikali.
Majaliwa
ametoa onyo hili katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika kata ya
Majimoto, Halmashauri ya Mpimbwe wilayani Mlele mkoani Katavi, kwamba
wananchi wanatakiwa kuwa macho na matapeli na mabilioni ya Magufuli.
“Serikali
haijaanza kusambaza fedha milioni 50 za JPM. Jihadharini na hao
matapeli na wezi hivyo wakija kwenye maeneo yenu wakamateni. Usambazaji
huo ukianza mtajulishwa kupitia halmashauri zenu,” aliwasisitiza.
Onyo
hilo la Waziri Mkuu, Majaliwa limekuja baada ya NEEC kutoa onyo kama
hilo kuhusu baadhi ya taasisi na watu binafsi wanawadanganya wananchi
kuwa fedha hizo zitapitia kwenye taasisi zao na kuwataka kujisajili nao
ili waweze kufaidika na fedha hizo, jambo ambalo si la kweli.
Katibu
Mtendaji wa Baraza hilo, Beng’i Issa amesema fedha hizo zimelenga
kukopesha vikundi vya wajasiriamali kupitia Vyama vya Ushirika vya Akiba
na Mikopo (Saccos) na vikundi vya kifedha vya kijamii zikiwamo Benki za
Maendeleo Vijijini (Vicoba) kwa ajili ya kuanzisha au kuendeleza
shughuli za kiuchumi.
Mpango
huo uliobatizwa jina la Fedha za Mfuko wa Mzunguko, unalenga
kukabiliana na tatizo la mitaji kwa ajili ya kuendesha shughuli za
kiuchumi kwa wananchi wanaoishi maeneo ya mijini na vijijini.
“Watu
na taasisi hizo zinazowadanganya wananchi zimekuwa zikiwatoza viwango
mbalimbali vya fedha kwa kile wanachodai ni ada ya usajili ili vikundi
hivyo vya wananchi viweze kusajiliwa na kutambuliwa kuweza kufaidika na
mamilioni hayo kwa kila kijiji,” anasema Issa.
Naibu
Waziri wa Kazi, Vijana na Ajira, Anthony Mavunde amesema ahadi ya Rais
ya Sh milioni 50 kwa kila kijiji itaanza kutekelezwa kwa mwaka wa
fedha wa 2016/2017.
Serikali
ya Awamu ya Tano imesisitiza kuwa itakuwa macho ili kuhakikisha fedha
hizo zinafanya kazi iliyokusudiwa na kuwafikia walengwa, ambao watakuwa
wamejiunga katika vikundi kama Saccos au Vicoba, wala si kila mtu mmoja
mmoja.
Hivyo
ili kupata mamilioni ya JPM ambaye ni rafiki wa watu masikini na
wajasiriamali kwa ujumla, Watanzania wote wana wajibu wa kufanya, ni
kujiunga katika vikundi na kuvisajili, ili vitambuliwe na vikubalike
kisheria. Vinginevyo itakuwa vigumu kufikiwa na mamilioni hayo.
MWISHO.
No comments:
Post a Comment