Social Icons

Monday, February 13, 2017

Asasi zaombwa kuingilia kati kukamatwa Watanzania Malawi



ASASI za kiraia, wabunge na vyombo vya habari vimeombwa kuingilia kati kukamatwa kwa Watanzania wanane nchini Malawi ambao ni watetezi wa haki za binadamu.
Watanzania hao kutoka Mtandao wa Kubadilishana Ujuzi na Kushirikishana taarifa katika masuala ya Kijamii, Kiuchumi na Mazingira (TUAM) uliopo Songea mkoani Ruvuma, walikamatwa Desemba 20, mwaka jana.
Mratibu wa Kitaifa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC), Onesmo Olengurumwa alisema Watanzania hao wamekamatwa na wanashitakiwa kwa mashitaka mawili ya kuingia nchini bila kibali (criminal trespass) na kupata taarifa bila kibali (carrying out reconnaissance).
Olengurumwa alisema watu hao hawakukusanya taarifa yoyote ambayo waliikusudia, kwa kuwa hawakufika eneo la tukio na kuelezea kuwa lengo la ziara hiyo ni kujifunza na kubadilishana uzoefu katika masuala ya mazingira na uchimbaji madini aina ya Urani.
“Watanzania waliokamatwa ni Briton Mgaya, Wakisa Mwansangu, Majidi Nkota, Christanduzi Ngowi, Ashura Kula, Martin Ndunguru, Wilbert Mahundi na Rainery Komba ambao awali walishitakiwa kwa makosa ya upelelezi lakini baadaye yalibadilishwa na kupewa mashitaka ya kuingia bila kibali na kupata taarifa bila kibali,” alisema Olengurumwa.
Alisisitiza watu hao wamekaa muda mrefu gerezani bila kesi yao kusikilizwa, hivyo serikali itoe amri ya kutaka watu hao waachiwe huru.
Naye Mwanasheria na Mkurugenzi wa Shirika la Haki za Binadamu na Biashara (BHRT), Flaviana Charles alisema Watanzania wanakabiliwa na mashitaka kinyume na Kifungu namba 314 (a) na 2 (3) ya Sheria ya Makosa ya Jinai ya Malawi pamoja na Kifungu namba 2 (4) cha Sheria ya Madini ya Malawi.
Charles alisema Watanzania hao, walikuwa wakielekea kijiji cha Karonga mpakani mwa Tanzania na Malawi kwa mwaliko wa asasi moja ijulikanayo kama Karonga Business Community ambayo iliratibu ziara hiyo kwa kushirikiana na Emmanuel Silungwe, mlinzi wa Kampuni ya uchimbaji urani ya Kayelekera Uranium Mine.
Pia alisema walituhumiwa kwamba Serikali ya Tanzania imewatuma kuipeleleza Malawi hususan kwenye masuala ya utengenezaji nyuklia, kitu ambacho si kweli na kwamba mashitaka yao yalibadilishwa zaidi ya mara nne kutokana na mwendesha mashitaka kutoona kosa la kuwashitaki nalo.
Hata hivyo, alisema kumekuwa na ukiukwaji wa haki za binadamu kwa kuwa mwanasheria na Ubalozi wa Tanzania nchini Malawi, walizuiwa kuwaona washitakiwa hao na baada ya mazungumzo ya muda mrefu ndio walikubali.
Alieleza kwamba mahojiano kati ya mwanasheria, watuhumiwa na ubalozi wetu walipoenda gerezani, yalifanyika chini ya ulinzi mkali ambao uliwafanya washitakiwa hao wasiwe na uhuru wa kujieleza.
CHANZO GAZETI LA HABARI LEO

No comments:

Post a Comment